Saturday, January 19, 2013

Ni kwa jinsi gani msomi anavyoweza kuleta mabadiliko chanya na pia kuleta hasara au kuwa chanzo cha matatizo ndani ya Jamii.


 Ni kwa jinsi gani msomi anavyoweza kuleta mabadiliko chanya na pia kuleta hasara au kuwa chanzo cha matatizo ndani ya Jamii.

Msomi ni mtu mwenye elimu ya jambo fulani. Katika nchi za kiafrika, kiwango cha elimu kimekuwa si cha kuridhisha ukilinganisha na nchi  zilizoendelea. Hali hii imezifanya serikali za nchi mbalimbali za kiafrika kutilia mkazo katika suala la elimu kwani elimu ni kiungo muhimu katika kufikia malengo ya maendeleo katika nchi yoyote duniani. Uchambuzi wa mada hii, unaegemea zaidi katika nchi zinazoendelea hasa za kiafrika na Tanzania ikiwemo.

Msomi anafaida kubwa na nafasi ya kuleta mabadiliko chanya ndani ya jamii. Umuhimu wa msomi ndani ya jamii ni pamoja na kufanya kazi mbalimbali za kitaalamu kama vile; udaktari, ualimu, uhandisi nk. Ufanyaji wa kazi hizi unapelekea kupata maendeleo na pia jamii kwenda sambamba na mabadiliko ya sayansi na technolojia.


Umuhimu mwingine wa msomi ni pamoja na kuwa mshauri ndani ya jamii katika mambo mbalimbali kama vile; kuwasadia wasio na elimu kwa kuwaelekeza njia bora za kufuata katika jambo fulani. Kwa mfano, msomi mwenye ujuzi na mambo ya kilimo, anaweza kuwashauri wakulima wanaomzunguka kufuata njia bora za kilimo kama vile kilimo cha kisasa. Kwa kufanya hivyo, msomi huyo, atakuwa anafaida kubwa katika jamii inayomzunguka.

Msomi pia anafaida kwani atakuwa ni motisha kwa jamii inayomzunguka. Hii ina maana kwamba, matendo mazuri atakayokuwa anayafanya msomi huyu, yatawapa motisha watu wengine ndani ya jamii kwa kuyaiga hivyo kuleta maendeleo ndani ya jamii husika. Kwa mfano, katika jamii za kijijini ambako kiwango cha elimu kipo chini, akitokea msomi ambaye amefanikiwa kutokana na elimu, basi inaweza kuwapa motisha watu wengine kuwapeleka shuleni watoto wao au wanafunzi wa eneo hilo kusoma kwa bidii ili kuwa kama yeye ambaye amefanikiwa kutokana na elimu.

Tukiachilia mbali faida za msomi, katika nchi za kiafrika zinazoendelea hasa Tanzania, msomi anaweza kuwa hatari na chanzo cha matatizo makubwa ndani ya jamii. Hii ina maana kwamba, msomi asiyemwaminifu anaweza kutumia elimu aliyonayo kuwadhulum na kuwaibia wanachi wasio na elimu badala ya kuwasaidia. Hali hii imefikia wasomi kuitwa “majambazi wa kalamu” Kwa mfano, hapa kwetu Tanzania, mtu akiwa anasoma anakwambia kabisa, akiajiriwa anachukua chake mapema na akiishaajiriwa anachukua chake mapema kwa kuiba au kuomba rushwa. Hali hii imepelekea wasomi wasiowaaminifu kuwa hatari na kukwamisha maendeleo  ya nchi.

Pia, baadhi ya wasomi wamekuwa chanzo cha matatizo ndani ya jamii ambapo wamekuwa wakitumia elimu yao kwa kuwarubuni au kuwadanganya watu wasio na elimu. Kwa mfano, msomi anaweza kuwashawishi wanajamii kutoshiriki jambo fulani lenye manufaa kama vile ujenzi wa shule na wanajamii nao watamsikiliza kutokana na imani ambayo bado imo miongoni mwa wanajamii wengi kwamba kile anachokisema msomi ni sahihi.

Matendo maovu ya msomi nayo yanaweza kuwakatisha tamaa wanajamii kwa kuona kuwa hakuna umuhimu wala maana ya kusoma endapo mtu anasoma halafu anafanya mambo yasiyo na tija katika jamii. Kwa mfano, unakuta msomi, anakunywa pombe halafu analala mtaroni, au unakuta msomi anatukana matusi ovyo barabarani au anaongea vitu visivyo na mantiki. Hali hii hupelekea wanajamii kuona kuwa hakuna tofauti kati ya aliyesoma na asiyesoma.

Hizi ni baadhi tu ya hasara na faida za msomi katika jamii. Hivyo basi, wewe kama msomi, unatakiwa uwe mfano mzuri wa kuigwa ndani ya jamii. Kumbuka kwamba, katika jamii yetu ambayo kiwango cha watu wenye elimu ni kidogo, bado msomi ana nguvu kubwa ya kuleta mabadiliko chanya au kuiharibu jamii.




 
Copyright © 2013. Mapalala Media